Friday 15 April 2016

Kigwangalla afanya ziara ya kushtukiza na kuzifunga Kliniki mbili

Naibu Waziri wa Afya Dk. Hamisi Kigwangalla (Kulia).

Naibu Waziri wa Afya,  Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto, Dk. Hamisi Kigwangalla amezifunga kiliniki mbili za Kikorea zinazotoa huduma ya tiba asili nchini kwa kosa la kutoa huduma bila ya kuwa na kibali pamoja na kuchanganya tiba asili, mbadala na ya kisasa pasipo Wizara ya Afya kuthibitisha kama vifaa inavyotumia vina ubora.
Aidha, Kliniki hizo zenye majina ya Korea Medical Clinic na Maibong Ukidar Medical zilizopo jijini Dar es Salaam zinatuhumiwa kutibu magonjwa ambayo katika usajili wake hayapo huku moja  ikitumia jina la CCM kama kinga ya kutofungiwa jambo lililopingwa vikali na Kigwangalla.
"Acha kusingizia kuwa kliniki yako ina uhusiano na CCM, usiichafue kwa kuwa haiko hivyo. Mimi mwenyewe ni mwanaccm sijapendezewa na kauli yako na ninakuagiza ulithibitishie baraza la tiba asili mmiliki halali wa kliniki hii na uache kutumia jina la CCM," amesema Kigwangalla.
Akizungumza wakati wa ukaguzi wa kliniki hizo, Kigwangalla ametoa agizo kwa Baraza la Usajili Tiba Asili nchini kuandika barua za kuzifunga kliniki hizo huku akimtaka msajili wa hospitali binafsi kufanya uchunguzi wa vifaa vinavyotumika katika kliniki hizo.

No comments: